Riba ya Benki Kuu yaongezwa hadi 6% kukabiliana na Mfumuko wa Bei

Katika hatua muhimu ya kukabiliana na shinikizo la mfumuko wa bei linalotokana na mwenendo wa uchumi duniani, Kamati ya Sera ya Fedha (MPC) imetangaza ongezeko la Kiwango cha Riba ya Benki Kuu (CBR) kutoka asilimia 5.5 hadi asilimia 6. 

Uamuzi huu, umefikiwa wakati wa kikao cha MPC kilichofanyika tarehe 3 Aprili 2024 kwa kuzingatia tathmini ya mwelekeo wa uchumi iliyofanyika mwezi Machi 2024.

Akitoa taarifa ya kamati hiyo katika Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya Benki Kuu Dar es Salaam mbele ya wakuu wa taasisi za fedha na vyombo vya habari, Gavana wa Benki Kuu Emmanuel Tutuba amesema marekebisho ya CBR yatakayotekelezwa kwa robo ya pili ya mwaka huu, yaani Aprili hadi Juni 2024, yamo ndani ya wigo wa asilimia 2 juu na chini. Hatua hii ya kujitolea inaonesha azma ya benki kuu katika kudumisha utulivu katikati ya mabadiliko ya uchumi.

“Uamuzi wa MPC wa kuongeza CBR unaonesha nia ya kudhibiti shinikizo la mfumuko wa bei katika mazingira mazuri ya kiuchumi,” amesema.

Tathmini ya MPC kuhusu hali ya uchumi duniani inaonyesha mwelekeo mzuri, huku uchumi wa nchi zilizoendelea na zinazoibukia ukiwa na utendaji bora. Ukuaji wa uzalishaji umekuwa zaidi ya matarajio, shinikizo la mfumuko wa bei limepungua. Hata hivyo, athari zinazoweza kusababishwa na maamuzi ya OPEC+ kuhusu uzalishaji wa mafuta na mivutano ya kisiasa ni eneo la wasiwasi.

Kitaifa, Gavana Tutuba amesema MPC imeridhika na utendaji wa uchumi licha ya changamoto za nje. 

“Kati ya mambo muhimu ni ukuaji imara wa Pato la Taifa wa asilimia 5.1 kwa mwaka 2023, uliochochewa na uwekezaji mkubwa wa sekta ya umma na binafsi, hususani katika miundombinu. Uchumi wa Zanzibar pia unaonyesha ukuaji mzuri, ukiongozwa na shughuli imara za utalii,” amesema.

Mfumuko wa bei, unaolingana na malengo, ulikuwa wastani wa asilimia 3.0 katika robo ya kwanza ya 2024, ukisaidiwa na sera madhubuti za fedha na upatikanaji wa chakula cha kutosha ndani ya nchi. Utekelezaji mzuri wa sera ya fedha umewezesha kiwango cha riba cha mikopo katika soko la benki kubaki ndani ya wigo uliopangwa na kuhimiza ukuaji imara wa mikopo kwa sekta binafsi.

Utendaji mzuri wa bajeti umehakikisha mapato yanakutana na matumizi yanalingana na rasilimali zilizopo, huku usawa wa biashara ukiendelea kuboresha kutokana na bei nzuri za uagizaji na utendaji mzuri wa mauzo nje.

Licha ya changamoto kama upungufu wa fedha za kigeni, hatua zinazoendelea za kuongeza usambazaji na kupunguza mahitaji ya dola ya Marekani yanatarajiwa kustawisha hali katika siku za karibu.

Akizungumza baada ya kutangazwa kwa CBR, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabenki Tanzania, Bw. Theobald Sabi, aliipongeza Benki Kuu ya Tanzania kwa kuja na kiwango hicho kinachozingatia mazingira ya sasa hivi. 

Pia aliishukuru Benki Kuu ya Tanzania kwa ushirikiano wake inaotoa katika maeneo mbalimbali yenye changamoto katika sekta ya mabenki, likiwezo tatizo la upatikanaji wa fedha za kigeni. 

"Hisia katika tasnia ya benki ni kwamba tunafurahishwa na kiwango cha ushirikiano na hatua jumuishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania," alisema Bw. Sabi. Pongezi kama hizo zilitolewa pia na mwakilishi wa Jumuiya ya Watoa Huduma za Mitandao ya Simu Tanzania (TAMNOA) na kueleza kwamba TAMNOA iko tayari kushirikiana na Benki Kuu kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.