Mfumo wa Sera ya Fedha

SERA YA FEDHA
Sera ya fedha inajumuisha hatua zinazochukuliwa na Benki Kuu ya Tanzania ili kubadili ujazi wa fedha na viwango vya riba. Hii hufanywa kwa kutumia nyezo za sera ya fedha ambazo Benki Kuu huona kuwa zinafaa kutumika kwa kipindi husika. 

Katika kutimiza jukumu hili, Benki Kuu hufanya tathimini ya hali ya uchumi na kuamua kiwango cha riba ya Benki Kuu kinachohitajika ili kufikia lengo la mfumuko wa bei unaozingatia ukuaji wa uchumi. Benki Kuu hutumia nyenzo mbalimbali za sera ya fedha ili kuhakikisha riba katika soko la fedha baina ya mabenki hapa nchini (interbank market rate) inakuwa tulivu sambamba na kiwango cha riba ya Benki Kuu. Benki Kuu hutumia riba za soko la fedha baina ya mabenki, kama lengo la uendeshaji ili kufikia malengo mapana ya kiuchumi. Katika shughuli zake za kila siku, Benki Kuu hutathimini hali ya ukwasi katika mfumo wa kibenki na kuamua kiasi, muda na aina ya vyenzo zitakazotumika katika usimamizi wa ukwasi.

MFUMO WA SERA YA FEDHA
Sera ya fedha ya Benki Kuu ya Tanzania hulenga kuthibibiti mfumuko wa bei nchini  na kuwezesha ukuaji endelevu wa uchumi kwa kuhahikisha kuwa riba za soko la fedha baina ya mabenki zinaendana na riba ya Benki Kuu. Mfumo huu wa sera ya fedha hujumuisha mambo yafuatayo:

Lengo la Sera ya Fedha  
Lengo la msingi la sera ya fedha ni kuhakikisha uwepo wa  utulivu wa bei, yaani kiwango kidogo na thabiti cha mfumuko wa bei. Mfumuko wa bei hupimwa kwa kuangalia mabadiliko ya kila mwaka katika fahilisi za bei. Katika kipindi cha muda wa kati (miaka 3-5), mfumuko wa bei unatarajiwa kuwa ndani ya wigo wa asilimia 5. Lengo hili linaendana  na vigezo vya jumuiya za kiuchumi za kikanda ambazo Tanzania ni mwanachama. Lengo hili pia ni sahihi kwa ajili ya kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi nchini. Hata hivyo, kutokana na athari za mitikisiko ya uchumi, mfumuko wa bei halisi unaweza kutofautiana na lengo kwa kipindi cha muda mfupi. Ili kufikia lengo hilo, Benki Kuu ya Tanzania hufuatilia kwa karibu ili kuhakikisha uwepo wa kiwango cha kutosha cha ukwasi katika uchumi pamoja na utulivu wa riba na  thamani ya shilingi ya Tanzania dhidi sarafu za nchi nyingine.

Lengo la Kati          
Benki Kuu hudhibiti mfumuko wa bei na kuwezesha ukuaji wa uchumi kwa kuamua  kiwango cha riba ya Benki Kuu. Riba hii hupangwa kuendana na matokeo ya mfumuko wa bei kama lengo la kati la sera hii, ambalo linaendana  na ukuaji endelevu wa uchumi.

Lengo la Uendeshaji        
Ili kufikia malengo ya mfumuko wa bei na ukuaji wa pato la Taifa, Benki Kuu huhakikisha kuwa viwango vya riba ya mikopo ya siku 7 katika soko la fedha baina ya mabenki (lengo la uendeshaji) vinaendana na riba ya Benki Kuu. Riba hii ya siku 7 kwenye soko la fedha baina benki imechaguliwa na  Benki Kuu kwa kuwa ni tulivu na ina uhusiano wa karibu na riba ya Benki Kuu.

Nyenzo za Sera ya Fedha
Benki Kuu ya Tanzania hutumia nyenzo mbalimbali za sera ya fedha ili kuhakikisha kuwa lengo la uendashaji linaendana na riba ya Benki Kuu. Aidha, kupitia nyenzo hizi, Benki Kuu hubadili ujazi wa fedha na gharama za mikopo katika uchumi. Nyenzo za msingi hujumuisha Benki kuu kuingia mikataba ya mauziano au manunuzi ya dhamana za muda mfupi na benki za biashara (repurchase agreement and reverse repurchase agreement) ili kuhakikisha kuwa kiwango cha ukwasi kinakuwa chenye kuridhisha. Nyenzo zingine ni pamoja na uuzaji na ununuzi wa  dhamana (debt securities), na uuzaji na ununuzi wa fedha za kigeni  katika soko la jumla la fedha za kigeni baina ya mabenki. Pia kiwango cha amana za benki  za biashara kinachotakiwa kuwekwa kisheria Benki Kuu (Statutory Minimum Reserve) na riba inayotumika kutoza benki za bishara au Serikali zinapochukua mikopo Benki kuu hutumika kama nyenzo za sera ya fedha. Pamoja na nyenzo hizo, Benki kuu pia hutoa mikopo ya muda mfupi ambayo hutakiwa kurudishwa ndani ya siku husika na ile ya siku moja (Intraday and Lombard loan facilities).Vilevile, Benki Kuu inaweza kutumia nyenzo nyingine za sera ya fedha kuendana na mahitaji.

Uwasilishaji wa Sera ya Fedha kwa umma    
Benki Kuu ya Tanzania inatekeleza jukumu lake la uandaaji na utekelezaji wa sera ya fedha kwa uwazi. Maamuzi ya Kamati ya Sera ya Fedha kuhusu riba ya Benki Kuu huwasilishwa kwenye mkutano wa Gavana na wakuu  wa taasisi za kibenki na pia huwasilishwa kwa umma kupitia vyombo vya habari. Vilevile, Benki Kuu huandaa na kuchapisha tamko la Kamati ya Sera ya Fedha na taarifa mbalimbali zinazoainisha mwelekeo wa sera ya fedha, matokeo utekelezaji wake na mwenendo wa uchumi kwa ujumla. Taarifa hizo zinapatikana kwenye tovuti ya Benki Kuu.